WAANDISHI WA HABARI WATANGAZA KUMCHUKULIA FOMU MWANDISHI MWENZAO JUVENTUS JUVENARY ILLAMBONA KUGOMBEA UDIWANI KATA YA KIBIMBA
Na, Bankanzako Ruguna
Ngara, Kagera – May 3, 2025
Kundi la waandishi wa habari kutoka wilayani Ngara mkoani Kagera limetangaza azma ya kumchukulia fomu ya kugombea nafasi ya Udiwani katika Kata ya Kibimba mwandishi mwenzao maarufu, Juventus Juvenary Illambona, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha ushiriki wa wanahabari katika uongozi wa kisiasa.

Uamuzi huo umetangazwa rasmi leo katika mkutano uliofanyika mjini Ngara, ambapo waandishi hao walieleza kuwa Illambona ni kiongozi mwenye maono, anayefahamu changamoto za wananchi wa Kibimba na mwenye uwezo wa kuibua na kusimamia maendeleo ya kata hiyo.
“Tumeamua kumchukulia fomu Juventus kama ishara ya imani yetu kwake. Amefanya kazi kwa ukaribu sana na jamii, anafahamu matatizo ya wananchi na ana uwezo mkubwa wa kuwasemea,” alisema mmoja wa waandishi hao, Godwin Bruchard, ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya kampeni hiyo.
Juventus Juvenary Illambona, ambaye ni mwandishi na mtangazaji wa wa muda mrefu kwenye kituo cha Redio Kwizera, na vyombo vingine vya habari, amepokelewa kwa shangwe na wakazi wa Kibimba baada ya taarifa hiyo kusambaa. Akizungumza kwa kifupi, Illambona alieleza kushukuru kwa heshima hiyo na kusema atatoa msimamo wake rasmi hivi karibuni.

Endapo atakubali ombi hilo, Illambona atakuwa miongoni mwa wanahabari wachache waliopata sapoti ya moja kwa moja kutoka kwa wanahabari wenzao kuingia kwenye siasa za moja kwa moja, hatua inayoashiria mabadiliko ya mtazamo kuhusu nafasi ya vyombo vya habari katika maendeleo ya jamii.
Mwanahabari mwingine nguli anayeshughulika na mitandao ya kijamii Baraka Silvanus Elia amesema ni muda sasa wa Wanahabari kuingia katika majukumu ya kiserikali wakitumia taaluma zao kurekebisha,kukosoa na kuwa mfano wa Uongozi.


